Maafisa wa Marekani na Ukraine wameanza mazungumzo leo Jumanne nchini Saudi Arabia huku upande wa Ukraine ukitarajiwa kuwasilisha sehemu ya mpango wa kusitisha mapigano na Russia.
Mpango wa Ukraine unajumuisha kusitisha mashambulizi ya makombora ya masafa marefu na sitisho la mapigano linalohusisha Black Sea. Hata hivyo Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy hakushiriki katika mikutano ya Jumanne, huku Ukraine ikiwakilishwa na mkuu wake Andriy Yermak, Waziri wa Mambo ya Nje wa Ukraine Andrii Sybiha, Waziri wa Ulinzi Rustem Umerov, na kamanda wa jeshi Pavlo Palisa.
Zelenskyy alisema katika mtandao wa X kabla ya mazungumzo kuanza kwamba ‘iko tayari kufanya kila kitu ili kufanikisha amani’. Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Marco Rubio, na mshauri wa usalama wa taifa Mike Waltz waliongoza ujumbe wa Marekani huku kukiwa na shinikizo la Rais Donald Trump la kutaka kumaliza haraka vita vilivyoanza mwanzoni mwa mwaka 2022 kwa uvamizi kamili wa Russia nchini Ukraine.
Rubio alisema Jumatatu kuwa Marekani inatarajia kutatua kizuizi cha kusitisha misaada kwa Ukraine.
Forum