Hii ni hatua ya kukabiliana na nchi hiyo baada ya kukaidi kusimamisha programu yake ya nyuklia na majaribio ya makombora, UN imesema.
Azimio hilo limeandaliwa na Marekani kwa kukabiliana na jaribio la sita la nyuklia lililofanywa na Pyongyang Septemba 3, ambalo linaaminika ni jaribio la kwanza la bomu la hydrojeni.
Rasimu hiyo ya kwanza imetaka Korea Kaskazini kuwekewa vikwazo vya nishati ya gesi na mafuta, pamoja na kukamatwa kwa rasilmali zake katika nchi za kigeni ambazo zinamilikiwa na kiongozi Kim Jong Un na serikali yake.
Wanadiplomasia sasa wanasema rasimu iliyorekebishwa italetwa Jumatatu ambayo imeboresha vikwazo vya mwanzo juu ya shehena za gesi na mafuta zinazosafirishwa, na inaondosha kukamatwa kwa rasilmali za Kim Jong Un.
Rasimu mpya imefikiwa baada ya majadiliano mazito yaliyojiri ikizihusisha nchi za Russia na China, ambazo zote zina kura ya veto katika Baraza hilo.
Rasimu hiyo mpya imesisitiza katazo la kusafirisha nje bidhaa za nguo ambalo lilikuwemo katika rasimu ya kwanza.
Korea Kaskazini imeonya mapema Jumatatu kwamba Marekani italipa “thamani kubwa” iwapo Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa litapitisha vikwazo dhidi ya Pyongyang.
“Dunia itashuhudia jinsi Jamhuri ya kidemokrasia ya Watu wa Korea Kaskazini itavyowadhibiti majangili wa Marekani kwa kuchukua hatua kadhaa ambazo ni nzito kuliko wao wanavyoweza kufikiria,” msemaji rasmi wa Pyongyang amesema.
Serikali ya Trump imesema hatua mbadala zote ziko mezani katika kukabiliana na Korea Kaskazini, likiwemo suala la kuchukua hatua za kijeshi. Rais ameonya kuwa tishio lolote linalofanywa na Korea Kaskazini dhidi ya Marekani na washirika wake litafuatiwa na hatua kali.